|
|
|
|
|
Mwanzo WakeJumuiya ya Sant'Egidio ilianzishwa mjini Roma mwaka 1968 kutokana na juhudi za kijana ambaye wakati huo alikuwa na umri chini ya miaka 20, jina lake Andrea Riccardi. Aliwakusanya pamoja vijana wenzake wanafunzi wa shule za Sekondari na kuanza kusoma na kujitahidi kuliishi Neno la Mungu maishani mwao. Mifano ya Jumuiya za kwanza za Kikristu katika Matendo ya Mitume, pamoja na maisha ya Mtakatifu Francis wa Assisi, ndivyo vilivyokuwa vielelezo muhimu kwa vijana hawa.
Kikundi hicho kidogo kilianza haraka kuenea katika mitaa ya Roma, wakitembelea makazi ya mabanda ambayo yalijaa watu maskini, na wakaanzisha shule za jioni (zilizojulikana kama "scuola popolare" yaani shule za watu, ama siku hizi "shule za amani") kwa ajili ya watoto.
Tangu wakati huo Jumuiya imeendelea kukua. Kwa sasa ipo katika nchi zaidi ya 60 katika Mabara manne. Idadi ya wanachama nayo imeendelea kuongezeka sambamba na ongezeko la idadi ya Jumuiya. Wapo duniani kote kadri ya wanachama 40,000 pamoja na wengine wengi ambao wanashiriki daima katika kazi ya kuwahudumia maskini na katika shughuli nyingine mbali mbali za Jumuiya ya Sant’Egidio. Pia kuna idadi kubwa ya watu wanaopokea huduma za aina mbalimbali ambazo Jumuiya hutoa.
|