|
"Kazi" ya pili ya Jumuiya, na pia nguzo yake ya pili ni uenezaji wa Injili. Injili yenyewe ndiyo kweli, habari njema tunayoweza kushirikiana na watu wengine; hazina ya thamani na mwanga usioweza kufichika. Injili siyo mali binafsi, ni jukumu kwa wanachama wa Jumuiya kutangaza Habari Njema kwa watu wengine. Tumeitwa kushirikiana hiyo Habari Njema.
Katika kuishi katika Jumuiya ya Sant’Egidio, kuwa mitume na kuishi kwa kushirikishana Injili ni neno moja. Ni jambo la furaha na la kusherehekea, kama tusomavyo katika Injili ya Luka wakati wale 72 waliporudi wakiwa wamejawa na furaha huku wakisema: "Bwana, hata mashetani wanatutii tunapolitumia jina lako" (Lk 10:17). Ni ushuhuda kwa kila mmoja wa wale wanafunzi na pia kila mwanachama wa Jumuiya ya Sant’Egidio, ambao umetuongoza katika miaka hii ya karibuni, kuweza kuishi "umisionari wa kindugu" katika sehemu nyingi za dunia.
|

|