|
|
|
|
Mwanzo Wake Jumuiya ya Sant'Egidio ilianzishwa mjini Roma mwaka 1968 kutokana na juhudi za kijana ambaye wakati huo alikuwa na umri chini ya miaka 20, jina lake Andrea Riccardi. Aliwakusanya pamoja vijana wenzake wanafunzi wa shule za Sekondari na kuanza kusoma na kujitahidi kuliishi Neno la Mungu maishani mwao. Mifano ya Jumuiya za kwanza za Kikristu katika Matendo ya Mitume, pamoja na maisha ya Mtakatifu Francis wa Assisi, ndivyo vilivyokuwa vielelezo muhimu kwa vijana hawa. Kikundi hicho kidogo kilianza haraka kuenea katika mitaa ya Roma, wakitembelea makazi ya mabanda ambayo yalijaa watu maskini, na wakaanzisha shule za jioni (zilizojulikana kama "scuola popolare" yaani shule za watu, ama siku hizi "shule za amani") kwa ajili ya watoto. Tangu wakati huo Jumuiya imeendelea kukua. Kwa sasa ipo katika nchi zaidi ya 60 katika Mabara manne. Idadi ya wanachama nayo imeendelea kuongezeka sambamba na ongezeko la idadi ya Jumuiya. Wapo duniani kote kadri ya wanachama 40,000 pamoja na wengine wengi ambao wanashiriki daima katika kazi ya kuwahudumia maskini na katika shughuli nyingine mbali mbali za Jumuiya ya Sant’Egidio. Pia kuna idadi kubwa ya watu wanaopokea huduma za aina mbalimbali ambazo Jumuiya hutoa. Sala "Kazi" ya kwanza kabisa ya Jumuiya ya Sant'Egidio ni sala. Kwa kusoma maandiko matakatifu vijana hao walipata changamoto ya kuishi maisha yao kikamilifu zaidi: waligundua mwito wa kuwa wafuasi, mwito ambao Yesu aliutangaza kwa vizazi vyote. Ni mwito wa kubadilisha maisha, kuacha kuishi kwa ajili ya mtu binafsi na kuanza kwa hiari kuwa chombo cha upendo mkubwa zaidi kwa watu wote, wanaume kwa wanawake, na hasa wale walio maskini zaidi. Kuishi na kusikiliza Neno la Mungu kama jambo la umuhimu zaidi katika maisha ina maana ya mtu kukubali kumfuata Yesu badala ya kufuata njia zake binafsi. Mfano halisi zaidi ni ile Jumuiya inayosali, iliyokusanyika pamoja kusikiliza Neno la Mungu. Ni kama ile familia ya wanafunzi waliomzunguka Yesu. Kuungana na kudumu katika sala (Matendo 2:42) ndiyo njia nyenyekevu inayokabidhiwa kama mfano na jukumu kwa wanachama wote wa Jumuiya ya Sant’Egidio. Sala ndiyo njia kuu ya kujiweka karibu na maneno ya Yesu na sala yake mwenyewe, na hata sala za vizazi vilivyopita, kwa mfano Zaburi, katika kuwasilisha kwa Bwana mahitaji ya watu maskini, mahitaji yetu wenyewe, na mahitaji ya ulimwengu nzima. Hii ndiyo maana, kule Roma, na katika miji mingine nchini Italia, Ulaya na kote duniani, Jumuiya zote hukusanyika mara nyingi iwezekanavyo kusali. Katika miji mingi kuna sala za pamoja ambazo ni wazi kwa kila mtu. Kila mwanachama wa Jumuiya anahitajika kujiwekea nafasi kwa ajili ya sala ya binafsi na kusoma Neno la Mungu peke yake katika maisha yake, akianzia na Injili. Uenezaji Injili "Kazi" ya pili ya Jumuiya, na pia nguzo yake ya pili ni uenezaji wa Injili. Injili yenyewe ndiyo kweli, habari njema tunayoweza kushirikiana na watu wengine; hazina ya thamani na mwanga usioweza kufichika. Injili siyo mali binafsi, ni jukumu kwa wanachama wa Jumuiya kutangaza Habari Njema kwa watu wengine. Tumeitwa kushirikiana hiyo Habari Njema. Katika kuishi katika Jumuiya ya Sant’Egidio, kuwa mitume na kuishi kwa kushirikishana Injili ni neno moja. Ni jambo la furaha na la kusherehekea, kama tusomavyo katika Injili ya Luka wakati wale 72 waliporudi wakiwa wamejawa na furaha huku wakisema: "Bwana, hata mashetani wanatutii tunapolitumia jina lako" (Lk 10:17). Ni ushuhuda kwa kila mmoja wa wale wanafunzi na pia kila mwanachama wa Jumuiya ya Sant’Egidio, ambao umetuongoza katika miaka hii ya karibuni, kuweza kuishi "umisionari wa kindugu" katika sehemu nyingi za dunia. Jumuia Isiyokuwa na Mipaka wala kuta Urafiki kati ya watu wa mataifa na mila tafauti ni njia ya kila siku ya kuendeleza undugu huu wa kimataifa katika Jumuiya ya Sant’Egidio. Ushirika huu wa kuishi pamoja kimataifa ina maana ya kuwa wazi kwa dunia nzima na pia kuishi katika familia moja, familia ya Mitume. Katika ulimwengu ambao mwisho wa milenia ya pili umezidisha vizingiti kati ya watu na kuchochea ubaguzi wa kitaifa na wa tofauti za mila na tamaduni, na ambayo ndiyo imekuwa chanzo cha migogoro mingi ya zamani na hata mipya. Jumuiya za Sant’Egidio zinashuhudia uwepo wa hatma sawa kwa watu wote, siyo tu kwa walio wakristu, bali kwa wanadamu wote. Zipo Jumuiya changa sana na pia kunazo zile za zamani zaidi. Nyingine zina idadi kubwa sana ya watu na mizizi iliyopenya zaidi kuliko nyingine; nyingine nazo zinajulikana zaidi kwenye mitaa au sehemu zilipo, lakini zote kwa pamoja zinajitahidi kuwa, na kwa kweli ni familia iliyomzunguka Yesu. Jumuiya ya Roma ndiyo Jumuiya kongwe zaidi ya zote. Ikiwa ni Jumuiya ya kwanza, inatoa huduma ya kuziweka pamoja zile Jumuiya changa bila kizingiti chochote "ila upendo" kama Baba Mtakatifu Yohane Paulo wa Pili alivyosema katika kumbukumbu ya miaka 25 ya Jumuiya ya Sant’Egidio mwaka 1993. Muungano huu unajieleza katika ushirika halisi na umoja kati ya ndugu, na ni muundo bora zaidi kwa maisha na shughuli za Jumuiya yenyewe. Urafiki na Watu Maskini "Kazi" ya tatu mahususi ya Jumuiya ya Sant’Egidio ambayo ni jukumu la kila siku tangu mwanzo ni utumishi kwa watu maskini, ambao pia ni wajibu wa kila siku tangu kuanzishwa kwake katika jukumu la kuishi urafiki. Vijana wanafunzi wa mwaka 1968 walioanza kukutana kwa ajili ya Neno la Mungu waligundua kwamba haingewezekana kamwe kuliishi mbali na watu maskini: watu maskini kama marafiki na Injili kama Habari Njema kwa watu maskini. Kwa njia hii Jumuiya ilianza huduma zake kabla haijapata jina la Sant’Egidio. Wakati huo iliitwa "shule ya watu" kwa sababu haikuwa tu inatoa elimu ziada kwa watoto wahama-shule wa mitaa ya mabanda (kwa mfano mabanda ya "Cinodromo" kando kando ya Mto Tevere) mjini Roma, bali ilikuwa ndio chanzo cha urafiki kati ya watu tajiri na wale maskini. Tangu wakati huo, "shule za watu" zilianza kukua na kuongezeka Roma na katika miji yote ambamo Jumuiya inaishi, huku umuhimu mkubwa ukipewa hasa kwa wale wanaoishi katika hali zilizo ngumu zaidi. Kuambatana na sura ya 25 ya Injili ya Mathayo, urafiki huu uliweza kusambaa hadi kwa watu wa namna nyingine za umaskini: viwete, watu wenye akili pungufu, wasio na makao, wahamiaji maskini kutoka nchi zingine, wagonjwa, kambi za Wagypsi na za wakimbizi. Kwa miaka hii iliopita, kumekuweko kutafakari zaidi juu ya hali za umaskini ambazo hazikuwepo, hasa katika nchi za Ulaya ambako kwa mfano, wazee huishi hali ya upweke hata kama wanazo mali. Jumuiya ya sant’Egidio hujiweka karibu na wale wanaochukuliwa kuwa duni zaidi, ikiwatambua kama ndugu pasipo ubaguzi wowote. Hao ni sehemu kamili ya Jumuiya. Kila palipo Jumuiya ya Sant’Egidio, kuanzia Roma hadi San Salvador, Cameruni hadi Ubelgiji, Ukraini hadi Indonesia, urafiki na kufahamiana na watu maskini zimekuwa daima shina lake. Hakuna Jumuiya, hata ile changa zaidi, ambayo ni ndogo au hafifu sana hata kutoweza kuwasaidia watu wengine maskini. Ni ile "hela ya mjane" iliyo na thamani kubwa zaidi mbele za Bwana (Mk. 12:41). Huduma kwa Ajili ya Amani: Kuifanya Dunia Kuwa na Ubinadamu Zaidi Urafiki na maskini iliifanya Jumuiya ya Sant’Egidio kutambua vyema zaidi kwamba vita ndiyo hasa mama wa umaskini. Kwa njia hii upendo kwa watu maskini katika hali nyingi tofauti uligeuka kuwa kuwa kazi ya kutafuta amani, kuilinda pale inapohatarishwa, na kusaidia kuijenga upya kwa kuhimiza moyo wa majadiliano popote pale ambapo imevunjika. Njia ifanikishayo huduma ya kuleta amani ni kwa kutumia nguvu hafifu ya sala, kushirikiana hali ngumu za maisha, kukutana na kujadiliana. Pia, pale ambapo hali iliyopo hairuhusu kazi hii ya kuleta amani, Jumuiya hujitahidi kuleta ushirikiano kindugu kupitia misaada ya kibinadamu kwa raia wa kawaida ambao ndio wanaoadhirika zaidi katika vita. Labda hizi ndizo sehemu ya shughuli za Sant’Egidio zinazofahamika zaidi, zinazozugumziwa sana kwenye vyombo vya habari. Lakini siyo mara nyingi utasikia vyombo hivyo vikitangaza shughuli zile za kindani za Jumuiya zinazotendeka daima za kufanya kazi pamoja na watu maskini, na kwamba Injili ndiyo mzizi wa kazi hizi. Wanachama wa Jumuiya waliweza pia kuwa wawezeshaji na wapatanishi wa mazungumzo ya amani nchini Mozambiko na pia Guatemala, ambako vita vya kimauaji vilidumu kwa zaidi ya miaka 30. Afrika na katika Balkan, na sehemu nyingine za Ulimwengu zilizojawa vita, zipo pia katika mawazo, nia na makusudio ya Jumuiya ya Sant’Egidio. Ilikuwa ni katika hali kama hizi ambapo imani ya Jumuiya ya Sant’Egidio katika "nguvu hafifu" ya sala na uwezo-kimapinduzi wa kuishi na kushawishi pasipo kutumia mabavu kutafuta amani ilipata kuzaliwa. Hizi ndizo fikra ambazo Yesu Kristu mwenyewe aliishi nazo hadi mwisho. Kwa sababu hii, Jumuiya daima hushughulikia huduma ya kuleta uwelewano na mazungumzo kati ya madhehebu na imani mbali mbali. Tangu 1987 Sant’Egidio imejitolea kuanzia mashinani hadi kiwango cha kimataifa katika kupanga mikutano ya kila mwaka, kongamano na mikutano ya sala katika "Moyo wa Assisi". Kwa kuitikia wito wa Assisi wa kulinda maisha katika hali zote, Jumuiya hii imejitolea katika kiwango cha kimataifa pamoja na mashirika mengine, kushughulikia shindikizo la kimataifa dhidi ya hukumu ya kifo katika mwaka wa 2000. Kampeni hii ni mnara mkubwa katika vita vya kulinda thamani ya uhai, na inawashirikisha wanachama wa Sant’Egidio kote ulimwenguni. Mzizi huu huu wa Injili ndio shina la mipango mingine ya kibinadamu ambako wito huwaendea watu wote wenye nia njema bila kujali imani zao. Hii inahusisha pia Kampeni dhidi ya mabomu ya kutegwa ardhini, misaada kwa wakimbizi na kwa waadhiriwa wa vita na njaa kusini mwa Sudan, Burundi, Albania na Kosovo, juhidi za kuwasaidia watu wa Amerika ya Kati walioadhiriwa vibaya na tufani, na pia dhidi ya biashara ya utumwa kokote inapofanyika. Jumuiya
ya Sant'Egidio |